Zakitaani Blog

Wednesday, February 13, 2013

AJALI MBAYA YA GARI

Watu wanane wamefariki dunia wakiwamo wanafunzi wanne wa shule ya sekondari na watatu kujeruhiwa baada ya gari walilokuwa wakisafiria aina ya Toyota Mark II kugongana na Mitsubishi Fuso eneo la Chalinze, mkoani Pwani.


Katika ajali hiyo iliyotokea juzi saa 12:00 jioni katika Kitongoji cha Kibiti Tarafa ya Chalinze, Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani, Mark II hiyo

yenye namba za usajili T. 363 AZG, iligongana uso kwa uso na Fuso yenye namba za usajili T. 433 AYQ.


Ajali hiyo ilitokea wakati Mark II iliyokuwa ikiendeshwa na Abuu Ahmed (21), kuwa katika mwendo kasi ikitokea Tanga kuelekea Morogoro kujaribu kulipita Fuso lililokuwa likitoka Morogoro kuelekea Dar es Salaam likiendeshwa na Mweta Daniel.


Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Pwani, Gregory Mushi, alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema kuwa waliokufa katika ajali hiyo ni wanafunzi wanne wa Shule ya Sekondari Chalinze wote wakazi wa eneo la Msolwa.


Aliwataja kuwa ni Essau Enos (16) wa kidato cha tatu, Latifa Shabani (17), wa kidato cha nne, Bahati George (18), wa kidato cha nne na Stella Isaack Kazimoto, (18).


Aliwataja watu wengine waliofariki dunia wakiwa katika Mark II kuwa ni Hassan Kulunga na Maria Sadick, wakazi wa Ubena ambao umri wao haukufahamika mara moja. Wengine ni dereva wa Mark II, Abuu Ahmed (21) na mtoto anayekadiriwa kuwa na umri wa kati ya miaka minne na mitatu aliyefahamika kwa jina la Samwel Ismail, ambaye ni mtoto wa marehemu, Maria Sadick. Aidha, Kaimu Kamanda huyo aliwataja majeruhi waliokuwa wamepanda Fuso kuwa ni William Thobias (30), mkazi wa Matombo mkoani Morogoro na utingo, Ahamad Juma (36).


Mushi alisema majeruhi hao wanaendelea na matibabu katika kituo cha afya Chalinze na miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali Teule ya Tumbi wilayani Kibaha. Ofisa Uhusiano wa Hospitali ya Tumbi, Rose Mtei, alithibitisha kupokea miili minane iliyokuwa imeharibika.


Kufuatia ajali hiyo, Kamanda Mushi ametoa wito kwa madereva kuzingatia sheria za usalama barabarani ili kuepuka ajali zinazotokea kwa uzembe na kwamba Jeshi la Polisi mkoa wa Pwani litawachukulia sheria kali madereva hao.


Shuhuda wa ajali hiyo, Godfrey Bonny, alisema ajali hiyo ilitokea wakati dereva wa Mark II akijaribu kulipita gari lililokuwa mbele yake ndipo gari lake lilipokutana uso kwa uso na Fuso.


“Mimi ni mkazi wa Chalinze, ilikuwa ni saa 12:30 jioni, nilisikia kishindo kikubwa na ndipo tulipokwenda katika eneo la tukio na kukuta gari dogo limeharibika vibaya na ikiwa chini ya uvungu wa gari kubwa. Lakini kutokana na kuchelewa kwa Kikosi cha Uokoaji, watu waliokuwamo ndani walipoteza maisha kwa kukosa msaada wa haraka,” alisema Bonny.


Shuhuda mwingine, Yusuph Mjema, ambaye pia ni mkazi wa Chalinze, alisema alipofika eneo la tukio, alikuta watu hao wamebanwa, lakini kutokana na kukosa vifaa maalum kwa ajili ya uokoaji, ilichukua muda mrefu kuwatoa.

No comments:

Post a Comment